Na, Edigar Nkilabo – SikongeDC
Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge inatarajia kuanza zoezi la umezeshaji dawakinga kwa magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele kwa Wanafunzi wa shule za Awali na Msingi wenye umri wa kuanzia miaka 5 hadi 14.
Hayo yamesemwa na Mratibu wa Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Sikonge Dkt.Mathew Sipemba katika kikao cha kujadili mpango mkakati wa kukabiliana na magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele.
“Magonjwa yasiyopewa kipaumbele ni mjumuiko wa magonjwa 21 tofautitofauti katika ukanda wa kitropikia Afrika,Asia na Amerika kusini, kwa Wilaya ya Sikonge mpango wa umezeshaji dawakinga kwa watoto ulianza mwaka 2016 na mwaka huu kuanzia tarehe 28 hadi 31 Januari, tutaanza zoezi hilo kwa Wanafunzi wote wa Awali na Msingi lengo ikiwa ni kudhibiti na kutibu magonjwa hayo” alisema Dkt.Sipemba.
Aidha Dkt.Sipemba amewatoa wasiwasi wazazi, walezi na walimu na kuwahakikishia kuwa dawakinga hizo ni salama na zipo za kutosha ikiwemo dawa aina ya Albendazole vidonge 79,600 ambazo zimeagizwa kutoka Bohari ya Taifa ya Dawa (MSD).
Kwaupande wake Mwenyekiti wa Kikao hicho Ndg.Andrea Ng’hwani amewataka Wataalam kuandaa utaratibu mzuri wa kuwafikia Watoto wote wenye umri wa kuanzia miaka 5 hadi 14 ili wapate dawakinga hizo.
“Najua kuanzia mwaka 2024 zoezi hili la umezeshaji dawakinga lilianza kuratibiwa na Halmashauri kupitia fedha za vituo vya kutolea huduma za afya, ni imani yangu jambo hili litatekelezwa kwa ufanisi na weledi kwa kuzingatia ushauri tulioutoa”alisema Ng’hwani.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri, Seif Salum amewataka Wataalam kutoa mafunzo kwa Walimu na wamezeshaji dawa,kufanya uhamasishaji katika jamii pamoja na kusimamia uandaaji wa taarifa.
Kikao hicho kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa hospitali ya Wilaya kimejumuisha Kamati ya Usalama ya Wilaya(KU), Wataalam wa Afya pamoja na Wakuu wa Vitengo na Divisheni kutoka Halmashauri kwa lengo la kujadili mpango mkakati wa utekelezaji wa zoezi hilo la umezeshaji dawakinga watoto wa umri wa miaka 5 hadi 14 Wilayani Sikonge
Mkurugenzi Mtendaji Sikonge DC
Anuani ya Posta: S.L.P 70 Sikonge, Tabora
Simu: 0767135460
Simu: 0767135460
Barua pepe: ded@sikongedc.go.tz
Hatimiliki ©2017Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, Haki zote zimehifadhiwa