SIKONGE WAPEWA WIKI MBILI KUJIBU HOJA ZOTE ZA CAG ZILIZOSABABISHA WAPATE HATI YENYE MASHAKA
NA EVELINA ODEMBA.
SERIKALI ya Mkoa wa Tabora imeiagiza Menejimenti ya Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge kuhakikisha ndani ya wiki mbili imemaliza kujibu hoja 68 za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zilizosalia ili ziweze kufutwa kwa kutoa vielelezo vinavyohitajika.
Agizo hilo lilitolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tabora Aggrey Mwanri wakati wa Kikao Maalumu cha Baraza la Madiwani cha kupitia hoja ya mbalimbali za Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa mwaka 2017/2018.
Alisema hoja hizo ndio zimesababisha Halmashauri hiyo kuwa kati ya Halmashauri saba nchini zilizopata Hati yenye shaka, ni lazima zijibiwe kwa kuwasilisha vielelezo vitakavyothibitisha matumizi ya fedha hizo kama yalifuata taratibu.
Mwanri aliwataka Wakuu wa Idara na Vitengo vya Halmashauri hiyo kuhakikisha wanatumia wiki hizo kutoa vielelezo ambavyo vitamwezesha Mkaguzi kufuta hoja.
Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa alimwagiza Katibu Tawala Mkoa wa Tabora kuhakikisha waliokuwa watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge ambao wamehamia Halmashauri nyingine na ambao wametajwa kwenye hoja za CAG warudishwe ili waje kujibu hoja.
Watumishi hao ni pamoja na aliyekuwa Mganga wa Wilaya (DMO), Afisa Utumishi (DHRO) na Mweka Hazina wa Wilaya(DT).
Alisema kwa kuwa watumishi hao wametajwa katika taarifa ni vema warudi ili waje kujibu hoja zao na kurudisha fedha ambazo zimeonyeshwa kwenye vitabu vya CAG.
Akisoma taarifa kwa niaba ya Mkaguzi Mkuu wa Nje, Christopher Chalo alizitaja sababu zilizopelekea kupata Hati yenye shaka kuwa ni pamoja na kutokuhakikiwa kwa vitabu 27 vya kukusanyia mapato, kuwepo kwa viashiria vya ubadhilifu katika matumizi ya fedha mbalimbali zenye thamani milioni 128,matumizi ya fedha za mapato ya ndani kabla ya kupelekwa Benki shilingi milioni 55.8.
Sababu nyingine ni fedha za EGPAF zilizotumika katika shughuli zisizojulikana kiasi cha milioni 73.2, fedha za posho zilizochukuliwa benki na kulipwa bila wahusika kukiri mapokezi milioni 29.3,kukosekana kwa hati za malipo za kiasi cha milioni 18.1.
Mwenyekiti wa Halmashauri ya Sikonge Mhe. Peter nzalalila akisoma dua maalum wakati wa baraza. pembeni ni Mkurugenzi wa Halmashauri Martha Luleka
Alisema sababu nyingine ni malipo yenye nyaraka pungufu kiasi cha milioni 15 na makusanyo ya papo kwa papo ambayo hayakupelekwa benki kiasi cha milioni 5.
Naye Katibu Tawala Mkoa wa Tabora Msalika Makungu alisema watawachukulia hatua watumishi wote ambao wameisababishia Halmashauri hiyo kuzalisha hoja za kiukaguzi za kiukaguzi na kupata Hati yenye shaka.
Alisema watumishi ni vema wakajitahidi kuzuia hoja na sio kutoa maamuzi ambayo yanasababisha kuendelea kuzalisha hoja kila mwaka .
Katibu Tawala Mkoa wa Tabora aliitaka Menejimenti ya Halmashauri hiyo kuunda timu ya kushughulikia hoja hizo ili ndani ya Mwezi mmoja wawe wamejibu na kufuta hoja hizo.
Makungu aliwaomba Madiwani kuhakikisha wanafuatilia katika Kata zao ili miradi mbalimbali ya wananchi iwe na ubora unaotakiwa.
Kwa upande wa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge Peter Nzalalila alisema wameunda timu ya Madiwani na Wataalamu watakaochunguza watendaji waliosababisha wapate Hati yenye shaka ili waweze kuchukuliwa hatua.
Mwisho
Mkurugenzi Mtendaji Sikonge DC
Anuani ya Posta: S.L.P 70 Sikonge, Tabora
Simu: 0767135460
Simu: 0767135460
Barua pepe: ded@sikongedc.go.tz
Hatimiliki ©2017Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, Haki zote zimehifadhiwa